Meta Yaanza Kutumia Chat za AI Kwenye Matangazo
Kampuni ya Meta imetangaza mabadiliko mapya yanayoanza kutumika Desemba mwaka huu, ambayo yataathiri watumiaji wa Instagram, Facebook na WhatsApp kote duniani isipokuwa katika nchi za Umoja wa Ulaya na Uingereza. Kwa mujibu wa Meta, data za mazungumzo unayofanya na Meta AI, ikiwemo pale unapoitumia kutafuta taarifa, kuomba muhtasari wa chat, kuuliza kuhusu bidhaa, au kutuma picha, zitaanza kutumika katika kufundisha mifumo yao ya AI pamoja na kubinafsisha matangazo utakayoyaona mtandaoni. Meta imeeleza kuwa mazungumzo ya kawaida kati ya watumiaji bado yapo kwenye mfumo wa end-to-end encryption, hivyo hawawezi kusoma ujumbe binafsi. Lakini pindi tu unapowasiliana na Meta AI, ndipo taarifa hizo zinachukuliwa kama sehemu ya data ambazo kampuni inaweza kuchakata. Wataalamu wa faragha wanasema mabadiliko haya yanaibua mjadala mpana kuhusu usalama wa taarifa binafsi, hasa kwa nchi ambazo hazina sheria kali za kulinda data. Kwa sasa, watumiaji hawana chaguo la kujitoa kwenye mfumo huu, isipokuwa kutotumia Meta AI kabisa. Meta inasema hatua hii inalenga kuboresha huduma za AI na kutoa matangazo yanayolingana zaidi na maslahi ya watumiaji.
Read More