
Bendi maarufu kutoka nchini Kenya Sauti Sol, imetishia kuchukua hatua za kisheria dhidi ya Chama cha Azimio la Umoja nchini humo kwa madai ya ukiukwaji wa hakimiliki.
Hatua hii inakuja baada ya muungano huo unaoongozwa na Raila Odinga kupiga wimbo wao wa ‘Extravaganza’ wakati wa hafla ya kumtambulisha Mgombea mwenza wa kiti cha urais, iliyofanyika Jumatatu hii katika ukumbi wa KICC.
Wakati wa hafla hiyo ya televisheni, Odinga alimtambulisha Mgombea mwenza Martha Karua huku ‘Extravaganza’ ikicheza nyuma, hatua ambayo bendi hiyo inasema haikuidhinishwa.
“Hatukutoa kibali cha wimbo huu kwa kampeni ya Azimio la Umoja walahatukutoa kibali chochote kwa matumizi yake katika kutangaza Mgombea wao wa Makamu wa Rais.”
Sauti Sol wamesema hawana misimamo yoyote ya kisiasa na kuahidi kuchukua hatua za kisheria dhidi ya timu inayoongozwa na Odinga kwa kukiuka haki miliki ya bendi hiyo.
Hata hivyo Raila Odinga kwa upande wake amesema wimbo huo ulipigwa kwa nia ya kuonesha upendo kwa sababu bendi hiyo imepeperusha bendera ya Kenya Kimataifa na Wakenya wanawashukuru kwa hilo.