
Shirikisho la Riadha Duniani limetangaza kuwa mabadiliko yamefanywa kwenye nyakati za kuanza kwa mashindano yote ya barabarani yatakayoandaliwa katika siku tatu za kwanza za Mashindano ya Riadha ya Dunia yatakayofanyika jijini Tokyo, Japan, kutokana na hali ya juu ya joto inayotarajiwa jijini humo ambayo inaweza kuhatarisha afya na usalama wa wanariadha.
Mashindano yaliyoathiriwa na mabadiliko haya ni pamoja na shindano la kutembea kilomita 35 kwa wanawake na wanaume litakalofanyika Jumamosi hii, pamoja na mbio za marathoni za wanaume zitakazofanyika Jumatatu ijayo. Mbio hizo sasa zitaanza dakika 30 mapema kuliko ilivyopangwa awali.
Katika taarifa ya pamoja, Shirikisho la Riadha Duniani pamoja na Kamati ya Maandalizi ya mashindano hayo wamesema hatua hiyo imechukuliwa kwa lengo la kutoa kipaumbele kwa afya na usalama wa wanariadha. Hata hivyo, nyakati za kuanza kwa mashindano ya ndani ya uwanja katika kipindi hicho bado hazijabadilishwa.
Mashindano ya Riadha ya Dunia ya mwaka huu yanatarajiwa kuanza rasmi Jumamosi hii jijini Tokyo.