Msanii wa Uganda Alien Skin Adaiwa Kukamatwa kwa Tu­huma za Mauaji

Msanii wa Uganda Alien Skin Adaiwa Kukamatwa kwa Tu­huma za Mauaji

Msanii mwenye utata kutoka Uganda, Alien Skin, ameripotiwa kuwekwa kizuizini baada ya kukamatwa mwishoni mwa juma kwa tuhuma za mauaji. Taarifa zinaeleza kuwa msanii huyo, ambaye ni bosi wa Fangone Forest, alinaswa na kikosi cha pamoja cha jeshi na polisi kilichozingira nyumba yake Jumamosi jioni. Inadaiwa kuwa katika upekuzi huo, maafisa wa usalama walikuta mapanga, upinde na mishale pamoja na silaha nyingine hatari nyumbani kwake, jambo lililoibua maswali zaidi kuhusu shughuli zake. Hata hivyo, vyombo vya usalama Uganda ikiwemo polisi na jeshi bado havijathibitisha rasmi kukamatwa kwake. Pamoja na hali hiyo, mashabiki wake wameanzisha kampeni mitandaoni wakitaka aachiliwe mara moja. Kwa mujibu wa mashabiki wake mitandaoni, kukamatwa kwake imehusishwa zaidi na kifo cha dansa mmoja maarufu wa Kampala ambaye alizikwa wiki iliyopita katika wilaya ya Mbale. Mashabiki wake wanadai msanii huyo ametupiwa lawama bila ushahidi wa moja kwa moja. Wakati huohuo, watumiaji kadhaa wa mitandao wamedai kuwa taarifa za kukamatwa kwake si za kweli, wakisisitiza kuwa Alien Skin yupo mafichoni na hajawahi kutiwa mbaroni. Madai ya kukamatwa kwa Alien Skin yameibuka saa chache tu baada ya Naibu Waziri wa Vijana nchini humo kuonya kuwa wasanii wanaoshirikiana na magenge ya kihalifu wako chini ya uchunguzi kwa makosa mbalimbali ikiwemo mauaji.

Read More
 Alien Skin Atangaza Kuacha Muziki Kufuatia Kesi ya Mauaji

Alien Skin Atangaza Kuacha Muziki Kufuatia Kesi ya Mauaji

Msanii mwenye utata kutoka Uganda, Alien Skin, amewashangaza mashabiki na wadau wa muziki baada ya kutangaza kujiondoa rasmi kwenye tasnia ya muziki kupitia TikTok Live. Alien Skin, ambaye ni bosi wa Fangone Forest boss, amesema amechoka na upinzani mkubwa anaoupata kutoka kwa wasanii wenzake na hata mashabiki, akifafanua kuwa hali hiyo imemuweka kwenye mawazo na msongo wa akili. Msanii huyo ambaye amekuwa kwenye sanaa kwa takriban miaka minne, amesema maadui zake wanajitahidi kila njia kumchafua, na kwa sababu hiyo ameamua kuacha muziki na kujikita kwenye maisha ya faragha Tangazo hilo limekuja wakati nyota huyo anakabiliwa na tuhuma nzito za mauaji. Jeshi la Polisi la Kampala Metropolitan limethibitisha kuwa linamchunguza Alien Skin na washirika wake kwa madai ya kuhusika katika kifo cha dansa Wilfred Namuwaya, maarufu Top Dancer. Inadaiwa kuwa Namuwaya alipigwa na kundi la washirika wa msanii huyo, hali iliyomsababishia matatizo ya kiafya na hatimaye kupelekea kifo chake mapema wiki hii. Msemaji wa Polisi, Patrick Onyango, amesema uchunguzi unaendelea na Alien Skin ndiye mtuhumiwa mkuu. Iwapo atapatikana na hatia ya kosa hilo la mauaji, anaweza kukabiliwa na kifungo cha maisha gerezani au hata adhabu ya kifo chini ya sheria za Uganda.

Read More