DCCAK Yamkemea Rigathi Gachagua kwa Kutaka Wasanii wa Mlima Kenya Wasusiwe

DCCAK Yamkemea Rigathi Gachagua kwa Kutaka Wasanii wa Mlima Kenya Wasusiwe

Chama cha Watayarishaji wa Maudhui ya Kidijitali Kenya (DCCAK) kimemkosoa vikali Naibu Rais wa zamani Rigathi Gachagua kufuatia wito wake wa kususia wasanii wa eneo la Mlima Kenya waliokutana na Naibu Rais Kithure Kindiki. Kupitia taarifa rasmi kwa vyombo vya habari, DCCAK ilieleza kuwa matamshi ya Gachagua ni ya kurudisha nyuma taifa na ni shambulio la moja kwa moja dhidi ya uhuru wa kujieleza, ubunifu, na biashara huru. “Tunapinga kwa kauli moja jaribio lolote la kuwanyamazisha wasanii kwa sababu ya maamuzi yao ya kibinafsi ya kisiasa. Huu ni ukiukaji wa haki za binadamu na uhuru wa kujieleza,” ilisomeka sehemu ya taarifa hiyo. Chama hicho kilisisitiza kuwa siasa haitakiwi kuwa kizuizi kwa maendeleo ya sekta ya burudani, na kuonya dhidi ya tabia ya kuwatisha wanamuziki na watayarishaji wa maudhui kwa misingi ya misimamo yao ya kijamii au kisiasa. Kauli ya DCCAK imekuja saa chache baada ya video kusambaa mtandaoni ikimuonesha Gachagua akiwashutumu wasanii waliokutana na Kindiki, akiwataka wakazi wa Mlima Kenya kuwasusia. Tukio hilo limezua mjadala mkali mitandaoni, huku wadau wengi wakimtaka Gachagua kuheshimu uhuru wa wasanii na kuacha kuingiza siasa katika masuala ya ubunifu.

Read More
 Terence Creative Ateuliwa Katibu Mkuu wa Chama cha Watayarishi wa Maudhui Mtandaoni Kenya (DCCAK)

Terence Creative Ateuliwa Katibu Mkuu wa Chama cha Watayarishi wa Maudhui Mtandaoni Kenya (DCCAK)

Mchekeshaji maarufu na mtayarishaji wa maudhui mtandaoni, Terence Creative, ametangazwa rasmi kuwa Katibu Mkuu (Secretary General) wa Digital Content Creators Association of Kenya (DCCAK) – chama kipya kinacholenga kutetea maslahi ya watayarishi wa maudhui nchini. Uteuzi huo ulifanyika katika hafla rasmi iliyowakutanisha wadau mbalimbali wa sekta ya kidijitali, ambapo pia walitambulishwa wajumbe wengine wa chama hicho, akiwemo Nasra Yusuff, Director Trevor, Sammy Kioko, na Claudia Naisabwa ambao watafanya kazi kwa karibu na Terence katika kuongoza harakati za chama hicho. DCCAK inalenga kuleta mabadiliko katika tasnia ya utayarishaji maudhui mtandaoni kwa kuweka sera bora, kushirikiana na serikali na sekta binafsi, pamoja na kutoa mafunzo, mikakati ya ukuaji, na ulinzi wa kazi za watayarishi. Akizungumza baada ya uteuzi wake, Terence alisema:  “Hii ni hatua kubwa siyo tu kwa mimi binafsi bali kwa jamii nzima ya watayarishi wa maudhui. Tunahitaji sauti ya pamoja ili kuhakikisha tunatambulika, tunalindwa, na tunapata mazingira bora ya kazi.” Watayarishi wa maudhui wameibuka kuwa sehemu muhimu ya uchumi wa kidijitali nchini Kenya, lakini wengi wao wamekuwa wakikabiliwa na changamoto za kisheria, kifedha na kimaudhui kutokana na kukosekana kwa mwongozo rasmi au uwakilishi thabiti. Kupitia uongozi wa Terence na timu yake, DCCAK inatarajiwa kuwa jukwaa la mabadiliko chanya katika uandaaji wa maudhui, kuendeleza vipaji vipya, na kuhimiza ubunifu unaozingatia maadili na haki za kiutendaji.

Read More