Telegram Yazindua Cocoon AI Isiyokusanya Data za Watumiaji
Kampuni ya Telegram imeamua kuingia kwenye ushindani mkali na Meta AI kwa kuzindua mfumo mpya wa akili bandia unaolenga kulinda faragha ya watumiaji. Hatua hii inalenga kuwavutia watumiaji ambao hawapendezwi na bidhaa za Meta, zinazokosolewa kwa kukusanya data binafsi za watumiaji. Telegram imeanzisha kipengele kipya kinachoitwa AI Summaries, kinachoendeshwa na akili bandia mpya iitwayo Cocoon. Kupitia Cocoon, watumiaji sasa wanaweza kufupisha ujumbe mrefu kwenye channels na kupata muhtasari kwa haraka na kwa urahisi zaidi. Kwa mujibu wa Telegram, Cocoon ni AI iliyojengwa kwa misingi ya faragha na usalama wa data. Kila ombi la mtumiaji hufichwa kwa mfumo wa encryption, na data hazionekani wala kuhifadhiwa na Telegram au wasimamizi wa Cocoon. Aidha, hakuna uhusiano kati ya maombi ya AI na utambulisho wa mtumiaji. Hatua hii inaonesha mwelekeo mpya wa Telegram wa kuimarisha ulinzi wa taarifa binafsi, huku ikizidi kuleta ushindani katika sekta ya akili bandia duniani.
Read More