Msanii Tipsy Gee Adai Wimbo Mpya wa Toxic Lyrikali Hauna Ubunifu

Msanii Tipsy Gee Adai Wimbo Mpya wa Toxic Lyrikali Hauna Ubunifu

Msanii anayesuasua kisanaa kutoka Kenya, Tipsy Gee, amemtolea uvivu rapa Toxic Lyrikali kwa kuuponda hadharani wimbo mpya wa rapa huyo uitwao “Euphoria.” Kupitia mitandao ya kijamii, Tipsy Gee ameonekana kutoridhishwa kabisa na ubora wa kazi hiyo, akisema kuwa wimbo huo haukidhi viwango vinavyotarajiwa kutoka kwa msanii ambaye sekta ya muziki inamtegemea. Tipsy Gee ambaye juzi kati aligeukia muziki wa Mugithi baada ya kushindwa kutamba na Arbatone, amesema kuwa haiwezekani msanii mwenye heshima kama Toxic Lyrikali kutoa wimbo ambao hauna ubunifu wala nguvu ya kushawishi mashabiki. Ikumbukwe, Tipsy Gee amekuwa mkosoaji mkubwa wa Toxic Lyrikali kwa muda sasa, kitendo ambacho wadau wa muziki nchini Kenya wanahoji kuwa huenda Titoker huyo aliyegeukia muziki anatumia jina la Lyrikali kujitengenezea nafasi katika tasnia ya muziki wa kizazi kipya.

Read More
 Msanii Tipsy Gee Amshutumu Militan wa Mbogi Genje kwa Kukata Dreadlocks za Parroty kwa Mabavu

Msanii Tipsy Gee Amshutumu Militan wa Mbogi Genje kwa Kukata Dreadlocks za Parroty kwa Mabavu

Msanii wa muziki wa Arbantone, Tipsy Gee, amezua mjadala mkali mtandaoni baada ya kumkemea vikali Militan, mmoja wa wanachama wa kundi la rap maarufu Mbogi Genje, kwa kile alichokiita kitendo cha kumvamia yeye na rafiki yake, Parroty, na kumnyoa dreadlocks zake kwa nguvu bila ridhaa yake. Tukio hilo lilitokea baada ya Parroty awali kuahidi kukata rasta zake endapo timu yake ya Manchester United ingefungwa na Tottenham Hotspur. Hata hivyo, licha ya Tottenham kushinda mechi hiyo, Parroty alibadilisha msimamo wake na kuomba msamaha kwa mashabiki, akisema kuwa angeacha kuishabikia Manchester United badala ya kukata rasta zake. Kwa mujibu wa Tipsy Gee, Militan alichukua sheria mkononi kwa kumshambulia Parroty na kumkata nywele bila makubaliano, kitendo ambacho kimezua hasira na lawama kutoka kwa wafuasi wa Parroty na wapenzi wa muziki wa mtaa. Mashabiki wengi wamejitokeza mitandaoni kulaani tukio hilo, wakilitaja kama ukiukaji wa haki ya mtu binafsi na ukosefu wa heshima. Wengine wameitaka Mbogi Genje kutoa msimamo rasmi kuhusu tukio hilo, huku wengine wakitaka hatua za kisheria zichukuliwe. Hadi sasa, Militan hajatoa tamko lolote rasmi kuhusiana na madai hayo. Tukio hili linaendelea kuzua mjadala mpana kuhusu mipaka ya mizaha, ahadi za mashabiki wa soka, na heshima kwa maamuzi ya mtu binafsi.

Read More
 Goddy Tennor Adai Kuwa Miongoni mwa Waanzilishi wa Miondoko ya Arbantone

Goddy Tennor Adai Kuwa Miongoni mwa Waanzilishi wa Miondoko ya Arbantone

Msanii na mtayarishaji wa muziki Goddy Tennor amedai kuwa yeye pamoja na wasanii wenzake Tipsy Gee, Soundcraft na Kappy ndio waanzilishi wa miondoko ya muziki wa Arbantone, mtindo unaozidi kushika kasi miongoni mwa vijana nchini Kenya. Akizungumza katika mahojiano maalum, Tennor alisema kuwa wazo la kuanzisha Arbantone lilizaliwa katika mazingira ya mtaa, likichochewa na haja ya kuwasilisha sauti ya vijana wa Nairobi kwa kutumia mitindo mipya ya midundo na lugha ya kizazi kipya. “Mimi, Tipsy Gee, Soundcraft na Kappy tulianzisha Arbantone. Tulikuwa tukikutana studio mara kwa mara tukijaribu vitu vipya hadi tukapata sound ya kipekee,” alieleza. Tennor aliongeza kuwa mtindo huo ulitokana na mchanganyiko wa muziki wa gengetone, trap, na midundo ya mtaa, na kwamba walilenga kuunda aina ya muziki unaoeleweka kitaifa lakini unaoweza kufika ngazi za kimataifa. Kwa mujibu wa Tennor, dhamira yao haikuwa kutafuta sifa, bali kuunda jukwaa la muziki ambalo lingebeba utambulisho wa vijana wa Nairobi. Alieleza kuwa mchanganyiko wa sauti ya mtaa na midundo ya kisasa ndio uliwapa msukumo wa kuunda aina hiyo ya muziki ambayo baadaye ilijulikana kama Arbantone. Hata hivyo, si kila mtu anakubaliana na kauli ya Tennor. Mwaka 2023, mtayarishaji maarufu Motif Di Don alidai kuwa ndiye mwanzilishi wa mtindo wa muziki unaofanana kwa jina tofauti la Urbantone. Ingawa Motif hakufafanua zaidi kuhusu mchango wa wasanii wengine, taarifa yake inaendelea kuibua mijadala kuhusu nani hasa alianza mtindo huo. Licha ya mvutano huo, Arbantone kwa sasa ni mojawapo ya mitindo ya muziki inayokua kwa kasi zaidi nchini. Mtindo huu umechangia kuibuka kwa wasanii kadhaa chipukizi ambao wanatawala majukwaa ya mitandao ya kijamii na redio. Miongoni mwao ni Maandy, YBW Smith, Soundkraft, Sean MMG, Lil Maina, Ebola Mkuu, Goddy Tennor mwenyewe, Kappy na Tipsy Gee. Muziki wa Arbantone umejipatia sifa kwa kuwasilisha maudhui ya maisha ya kila siku ya vijanakutoka kwenye uhusiano wa kimapenzi hadi changamoto za kijamii kwa lugha ya mtaa inayovutia hadhira kubwa. Wachambuzi wa muziki wanasema kuwa mvutano kuhusu nani aliyeanzisha Arbantone ni wa kawaida katika hatua za awali za maendeleo ya mtindo wowote mpya. Hata hivyo, wanakubaliana kuwa miondoko hiyo imefungua ukurasa mpya katika muziki wa Kenya na huenda ikawa sehemu ya utambulisho wa muziki wa kisasa Afrika Mashariki kwa miaka mingi ijayo.

Read More