Eddy Kenzo Kutatua Mgogoro wa Ofisi za UMA Zilizofungwa kwa Madeni

Eddy Kenzo Kutatua Mgogoro wa Ofisi za UMA Zilizofungwa kwa Madeni

Rais wa Shirikisho la Wanamuziki Uganda (UNMF) na mshauri wa Rais wa Jamhuri ya Uganda katika masuala ya ubunifu, Eddy Kenzo, ameahidi kuingilia kati na kusaidia Chama cha Wanamuziki Uganda (UMA) kurejeshewa ofisi zake zilizofungwa kutokana na deni la kodi. Kwenye mahojiano na kituo kimoja cha runinga nchini humo, Kenzo amesema hatua hiyo inalenga kutunza heshima ya taasisi ya UMA ambayo, kwa mujibu wake, imekuwa na mchango mkubwa katika maendeleo ya muziki nchini Uganda kabla ya kuanzishwa kwa UNMF. “Hatuwezi kuwaacha katika hali hii. UMA walifanya kazi kubwa kabla sisi hatujaja. Tutaingilia kati na kuona namna ya kuhakikisha ofisi zao zinafunguliwa tena,” alisema Kenzo katika mahojiano na kituo cha televisheni cha ndani. Kauli yake imekuja kufuatia hatua ya Kituo cha Kitaifa cha Utamaduni cha Uganda (UNCC), kinachomiliki jengo la National Theatre, kufunga rasmi ofisi za UMA kwa kile kilichoelezwa kuwa malimbikizo ya kodi ya karibu mwaka mmoja. Hatua hiyo imeathiri moja kwa moja uendeshaji wa shughuli za chama, huku ofisi za viongozi wakuu kama Cindy Sanyu (Rais wa UMA) na Phina Masanyalaze (Katibu Mkuu) zikiwa zimefungwa na kuwekewa zuio la kuingia. UMA, chini ya Cindy, imekuwa ikikosoa waziwazi uongozi wa UNMF na haswa Kenzo, huku mvutano kati yao ukijidhihirisha mara kadhaa katika majukwaa ya umma. Hata hivyo, Kenzo amechukua hatua ya kukutana na viongozi husika ili kushughulikia suala hilo kwa njia ya amani, akisema huu si wakati wa kutazama tofauti bali kushikamana kwa maslahi ya wanamuziki wote nchini Uganda. Sakata hili linaendelea kuwavutia wadau wengi wa sekta ya burudani nchini Uganda, huku wengi wakisubiri kuona ikiwa hatua ya Kenzo itazaa matunda na kumaliza mgogoro unaoathiri ustawi wa chama kongwe cha wanamuziki nchini.

Read More
 Nina Roz Afichua Sababu za Kujiondoa UNMF, Amsuta Vikali Eddy Kenzo kwa Kuwa Mbinafsi

Nina Roz Afichua Sababu za Kujiondoa UNMF, Amsuta Vikali Eddy Kenzo kwa Kuwa Mbinafsi

Mwanamuziki maarufu na mwanasiasa chipukizi, Nina Roz, ameibua mjadala mpya katika tasnia ya muziki nchini Uganda baada ya kufichua sababu zilizomfanya kujiondoa kwenye Shirikisho la Kitaifa la Wanamuziki nchini humo (UNMF) Katika mahojiano aliyofanya hivi karibuni na vyombo vya habari, Nina Roz alieleza kuwa walibuni shirikisho hilo pamoja na  Eddy Kenzo kwa madhumuni ya kuwatetea wasanii, kusimamia haki zao, na kuendeleza ustawi wa sekta ya muziki nchini Uganda. Hata hivyo, alidai kuwa hali hiyo ilianza kubadilika muda mfupi baada ya kuanzishwa kwa shirikisho hilo mwaka 2023.  “Nilidhani tunaunda jukwaa la kweli la kuwaunganisha wasanii na kuwatetea, lakini baadaye nikabaini kuwa viongozi, hususan Eddy Kenzo, walikuwa na maslahi binafsi pamoja na ajenda za kisiasa ambazo hazikuwiana na malengo ya awali,” alisema Nina Roz. Nina, ambaye aliwahi kushika wadhifa wa kusimamia masuala ya maadili ndani ya UNMF, alieleza kuwa shirikisho hilo lilianza kupoteza dira na kuonyesha ukaribu usiofaa na serikali. Kwa maoni yake, hali hiyo ilikuwa kinyume na misingi ya uhuru wa kujieleza na uhuru wa kisanii. Tangu kujiondoa kwake, Nina Roz amekuwa mkosoaji wa wazi wa shirikisho hilo, akilituhumu kwa kile alichokitaja kuwa ni siasa za upendeleo katika tasnia ya muziki. Anadai kuwa wasanii wanaoonekana kukosoa serikali wamekuwa wakibaguliwa katika upatikanaji wa fursa, mikataba, na msaada kutoka kwa taasisi hiyo. “UNMF haikuwakilisha tena maslahi ya wasanii wote. Iligeuka kuwa jukwaa la upande mmoja, ambapo wale waliokuwa karibu na serikali ndio walipewa kipaumbele,” aliongeza. Kwa sasa, Nina Roz anajiunga na orodha ya wasanii wakubwa kama King Saha, Ziza Bafana, na Spice Diana, ambao wote wamejitenga na UNMF, wakieleza kutoridhishwa  na namna taasisi hiyo inaendeshwa.

Read More