Spice Diana Afichua Mbinu Aliyotumia Kukwepa Rushwa ya Ngono
Msanii nyota wa muziki kutoka Uganda, Spice Diana, amefunguka kuhusu changamoto alizokumbana nazo mwanzoni mwa safari yake ya muziki, akieleza namna alivyokwepa wanaume waliotaka kutumia nafasi zao kumshawishi kwa rushwa ya ngono. Akizungumza katika mahojiano na kituo kimoja cha televisheni nchini Uganda, Spice Diana amesema katika kipindi ambacho alikuwa bado anatafuta mafanikio kwenye tasnia ya muziki, alikutana na watu kadhaa waliomfuata wakiahidi kumsaidia kukuza kazi yake ya muziki kwa masharti ya mahusiano ya kimapenzi. Msanii huyo ambaye amedumu katika tasnia ya burudani kwa takribani miaka 15, amesema wengi wa watu hao walijitambulisha kama mameneja wa muziki au mapromota waliodai kuwa na uwezo wa kumfungulia milango ya mafanikio. Hata hivyo, Spice Diana amesema alitumia mbinu ya kipekee ili kujilinda dhidi ya shinikizo hilo. Amesema aliwageuza wanaume wote waliomfuata kwa nia hizo kuwa marafiki wa kawaida badala ya kukubali mahusiano ya kimapenzi waliyojaribu kumlazimisha. Kwa mujibu wa msanii huyo, mbinu hiyo haikuwa rahisi kwa baadhi yao, lakini ilimsaidia kuendelea kujenga kazi yake ya muziki bila kukubali masharti aliyoyaona si sahihi. Spice Diana pia ameonya kuwa hali kama hiyo mara nyingi huwakumba wasanii chipukizi wa kike ambao bado wanatafuta nafasi ya kung’ara kwenye tasnia ya muziki, huku baadhi ya watu wakitumia udhaifu huo kujaribu kuwashawishi kwa ahadi za mafanikio.
Read More