William Saliba Kukaa Arsenal Mpaka 2030 Baada ya Kukubali Mkataba Mpya

William Saliba Kukaa Arsenal Mpaka 2030 Baada ya Kukubali Mkataba Mpya

Beki wa klabu ya Arsenal na timu ya taifa ya Ufaransa, William Saliba, ameripotiwa kukubali kusaini mkataba mpya wa miaka mitano na miamba hiyo ya Ligi Kuu ya England (EPL), hatua itakayomuweka Emirates hadi mwaka 2030. Saliba, ambaye amekuwa nguzo muhimu katika safu ya ulinzi ya Arsenal, alikuwa amesalia na miaka miwili kwenye mkataba wake wa sasa unaotarajiwa kumalizika mwezi Juni 2027. Hata hivyo, uongozi wa Arsenal umeamua kumfunga kwa muda mrefu zaidi, kufuatia kiwango chake bora ambacho kimevutia vilabu vikubwa barani Ulaya, ikiwemo Real Madrid ya Uhispania. Kwa mujibu wa duru za ndani ya klabu hiyo ya Kaskazini mwa London, mkataba huo mpya unatarajiwa kutangazwa rasmi katika siku chache zijazo, huku mashabiki wakitarajia kuendelea kumuona beki huyo mwenye kasi na akili ya mchezo akiwa sehemu ya kikosi cha kwanza kwa miaka mingi ijayo. Tangu kurejea kutoka kwa mkopo msimu wa 2022/23, Saliba amekuwa mchezaji wa kuaminiwa na kocha Mikel Arteta, akicheza nafasi ya beki wa kati kwa utulivu mkubwa, na kushirikiana kwa mafanikio na Gabriel Magalhães katika safu ya ulinzi.

Read More
 TikTok Yaanzisha Mfumo wa Kuchangisha Michango kwa Watumiaji

TikTok Yaanzisha Mfumo wa Kuchangisha Michango kwa Watumiaji

TikTok, jukwaa maarufu duniani kwa kushiriki video fupi, limeanzisha mfumo mpya utakaowawezesha watumiaji wake kuchangisha michango moja kwa moja kupitia akaunti zao. Hatua hii inalenga kuwawezesha wabunifu wa maudhui (content creators) kupata usaidizi wa kifedha kutoka kwa mashabiki wao, hasa katika nyakati ambazo wanahitaji msaada au wanapofanya kazi za kijamii na kijamii. Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na kampuni hiyo, mfumo huu mpya wa uchangishaji utapatikana kupitia kipengele maalum kitakachowekwa kwenye wasifu (profile) wa mtumiaji, ambapo mashabiki wataweza kuchangia kwa hiari fedha zao kwa kutumia njia salama za malipo mtandaoni. TikTok imesema kuwa lengo la huduma hiyo ni kusaidia kukuza vipaji na kusaidia watumiaji wanaotegemea jukwaa hilo kama chanzo cha kipato, hasa wale wanaohusika na harakati za kijamii, kazi za hisani au hata gharama za kibinafsi kama vile matibabu, elimu, au miradi ya ubunifu. Kampuni hiyo imeweka masharti na vigezo vya nani atakayestahiki kutumia kipengele hicho, ikiwa ni pamoja na kuwa na idadi fulani ya wafuasi, umri unaokubalika, na kuzingatia maadili ya matumizi ya TikTok. Hata hivyo, TikTok imeahidi kuweka mifumo madhubuti ya kuchuja na kufuatilia namna huduma hiyo itakavyotumika, huku ikisisitiza kuwa itahakikisha uwazi, usalama na matumizi sahihi ya mfumo wa kuchangisha michango.

Read More
 Joel Lwaga Asaini Mkataba na Empire Africa

Joel Lwaga Asaini Mkataba na Empire Africa

Mwimbaji wa nyimbo za Injili kutoka Tanzania, Joel Lwaga, ametangaza rasmi kusaini mkataba wa usambazaji wa muziki na kampuni kubwa ya kimataifa, Empire Africa. Hatua hii imeonekana kama mwanzo mpya wa ushirikiano wa kibiashara ambao unatarajiwa kupeleka muziki wake katika viwango vya juu zaidi na kumfikisha kwa mashabiki wengi duniani. Kama ishara ya mwanzo wa safari hii mpya, Lwaga ameachia wimbo wake mpya unaoitwa “Saa Hii”, ambao tayari upo kwenye majukwaa yote ya kidigitali duniani. Wimbo huo unakuja na ujumbe wa imani na matumaini, ambao ni utambulisho wa kipekee wa muziki wa Joel Lwaga. Mashabiki wake wamepokea kwa furaha tangazo hilo, wakieleza matumaini makubwa kwamba ushirikiano huu na Empire Africa utaleta mafanikio makubwa zaidi kwa msanii huyo anayejulikana kwa sauti yake yenye kugusa mioyo na nyimbo zenye ujumbe wa kiroho. Kwa kusaini mkataba huu, Joel Lwaga anaungana na orodha ya wasanii kutoka barani Afrika wanaofanya kazi na Empire Africa, kampuni ambayo inajulikana kwa kufanikisha kazi za wasanii katika soko la kimataifa.

Read More
 Bahati Awahimiza Wanaume Kuachia Wake Zao Mali Ndoa Inapovunjika

Bahati Awahimiza Wanaume Kuachia Wake Zao Mali Ndoa Inapovunjika

Msanii wa muziki wa Kenya, Bahati, ameibua mjadala mtandaoni baada ya kuwataka wanaume waachie wake zao mali na kila kitu iwapo wataachana au kupeana talaka. Akizungumza katika mahojiano yaliyosambazwa kwenye mitandao ya kijamii, Bahati amesisitiza kuwa amani ya moyo na kuanza upya ni jambo la maana zaidi kuliko kushikilia mali au vitu vya kidunia. Kwa mujibu wa msanii huyo, ni bora mwanaume aondoke mikono mitupu lakini akiwa na utulivu wa nafsi, kuliko kuingia kwenye malumbano yasiyoisha kuhusu mgawanyo wa mali. Bahati, ambaye mara nyingi huzungumza kwa ujasiri kuhusu masuala ya ndoa na mahusiano, amesema kuwa wanaume wanaojikuta wakipigania mali huishia kuchoshwa kiakili na kifedha. Hata hivyo amewashauri badala yake wajikite katika kujijenga upya na kusonga mbele. Kauli hiyo imezua maoni tofauti miongoni mwa mashabiki. Baadhi wamepongeza msanii huyo kwa kuhimiza amani na ukomavu, huku wengine wakisema wanaume nao wanastahili haki na si sahihi kuondoka bila chochote walichokifanyia kazi.

Read More
 Vera Sidika Amchana Eddie Butita Kuhusu Kauli za Boo Party

Vera Sidika Amchana Eddie Butita Kuhusu Kauli za Boo Party

Socialite wa Kenya Vera Sidika ameonekana kuchukizwa na matamshi ya mchekeshaji Eddie Butita aliyewakosoa wanaume waliohudhuria hafla yake ya hivi karibuni maarufu kama Boo Party. Kupitia video aliyoipakia mitandaoni, Vera amemshutumu Butita kwa kuwa na machungu kwa sababu hakupata mualiko wa kushiriki sherehe hiyo. Amesema hakuna mwanaume timamu ambaye angekataa mwaliko wa hafla kama hiyo, akidai ni wachache tu wenye majungu na wivu wanaoweza kutoa maneno ya kubeza. Aidha, amemshauri Butita kuacha kufuatilia maisha yake na kuacha majungu, akibainisha kuwa siku zijazo huenda akampatia mualiko rasmi ili ahudhurie moja ya sherehe zake. Mapema wiki hii, Vera alifanya Boo Party maalum kwa ajili ya kusherehekea hatua yake ya upasuaji wa urembo, baada ya kufanikisha kuongeza uthabiti wa matiti yake. Hafla hiyo ilivutia hisia tofauti mitandaoni, huku baadhi ya mashabiki wakimpongeza na wengine wakibeza. Kulingana na Butita, hakuelewa sababu ya wanaume kushiriki hafla ya aina hiyo.Alisema kwamba ilikuwa sawa kwa marafiki wa kike wa Vera kumuunga mkono, lakini aliona haikuwa na mantiki kwa wanaume kuhudhuria tukio lililolenga kusherehekea upasuaji wa mwili.

Read More
 Alien Skin Atangaza Kuacha Muziki Kufuatia Kesi ya Mauaji

Alien Skin Atangaza Kuacha Muziki Kufuatia Kesi ya Mauaji

Msanii mwenye utata kutoka Uganda, Alien Skin, amewashangaza mashabiki na wadau wa muziki baada ya kutangaza kujiondoa rasmi kwenye tasnia ya muziki kupitia TikTok Live. Alien Skin, ambaye ni bosi wa Fangone Forest boss, amesema amechoka na upinzani mkubwa anaoupata kutoka kwa wasanii wenzake na hata mashabiki, akifafanua kuwa hali hiyo imemuweka kwenye mawazo na msongo wa akili. Msanii huyo ambaye amekuwa kwenye sanaa kwa takriban miaka minne, amesema maadui zake wanajitahidi kila njia kumchafua, na kwa sababu hiyo ameamua kuacha muziki na kujikita kwenye maisha ya faragha Tangazo hilo limekuja wakati nyota huyo anakabiliwa na tuhuma nzito za mauaji. Jeshi la Polisi la Kampala Metropolitan limethibitisha kuwa linamchunguza Alien Skin na washirika wake kwa madai ya kuhusika katika kifo cha dansa Wilfred Namuwaya, maarufu Top Dancer. Inadaiwa kuwa Namuwaya alipigwa na kundi la washirika wa msanii huyo, hali iliyomsababishia matatizo ya kiafya na hatimaye kupelekea kifo chake mapema wiki hii. Msemaji wa Polisi, Patrick Onyango, amesema uchunguzi unaendelea na Alien Skin ndiye mtuhumiwa mkuu. Iwapo atapatikana na hatia ya kosa hilo la mauaji, anaweza kukabiliwa na kifungo cha maisha gerezani au hata adhabu ya kifo chini ya sheria za Uganda.

Read More
 Dulla Makabila Asema Waganga Ndio Nguzo Ya Safari Yake Ya Muziki

Dulla Makabila Asema Waganga Ndio Nguzo Ya Safari Yake Ya Muziki

Msanii wa Singeli kutoka Tanzania, Dulla Makabila, amefichua kuwa siri ya juhudi zake kwenye muziki haina uhusiano mkubwa na kipaji, bali nguvu anazoweka kwa waganga. Kupitia maelezo yake, Dulla amesema kuwa amekuwa akielewa mapema kuwa hana kipaji kikubwa cha kuwavutia mashabiki kama wasanii wengine, hivyo ameamua kuwekeza zaidi katika njia za kiimani na kiutamaduni ili kuhakikisha safari yake ya muziki inasonga mbele. Aidha, msanii huyo anasisitiza kuwa licha ya changamoto nyingi anazokutana nazo, anaamini msaada wa waganga unamuweka katika nafasi ya kupambana na kuendelea kushikilia jina lake katika tasnia ya Singeli. Kauli ya Dulla imeibua gumzo miongoni mwa mashabiki wa muziki, baadhi wakionesha mshangao huku wengine wakisema kwamba kila msanii ana mbinu na imani zake za kusimama kwenye muziki.

Read More
 Daddy Owen Afunguka Kuhusu Tukio Lililomvunja Moyo Akiwa Kwenye Kilele cha Umaarufu

Daddy Owen Afunguka Kuhusu Tukio Lililomvunja Moyo Akiwa Kwenye Kilele cha Umaarufu

Msanii wa nyimbo za injili nchini Kenya, Daddy Owen, amesimulia kisa cha kusikitisha alichowahi kupitia akiwa kwenye kilele cha umaarufu kisanaa. Akiwa kwenye mahojiano hivi karibuni, Owen ameeleza jinsi alivyokuwa amialikwa kutumbuiza katika shule moja ya wasichana, lakini aliposhika jukwaa, wanafunzi wote walitoka ukumbini na kumwacha peke yake. Tukio hilo lilisababishwa na tetesi zilizokuwa zikienea wakati huo zikimhusisha na ibada za kishetani. Daddy Owen amesema kitendo hicho kilimuumiza, lakini kilimjenga na kumpa moyo wa kuendelea na huduma yake ya injili kupitia muziki. Ameongeza kuwa changamoto kama hizo ni sehemu ya safari ya imani na sanaa, akisisitiza umuhimu wa kusimama imara licha ya madai ya uongo. Kisa hicho kilitokea wakati msanii huyo alikuwa kwenye kilele cha muziki wake, ambapo vibao vyake maarufu kama System ya Kapungala na Tobina vilikuwa vikivuma sana na kumpa umaarufu mkubwa nchini. Licha ya changamoto hizo, Daddy Owen ameendelea kung’ara kama mmoja wa wanamuziki wa injili wenye ushawishi mkubwa nchini, akiwa na nyimbo nyingi zenye ujumbe wa matumaini na uvumilivu.

Read More
 Cindy Sanyu Avunja Ukimya Kuhusu Pete ya Ndoa

Cindy Sanyu Avunja Ukimya Kuhusu Pete ya Ndoa

Mwanamuziki nyota kutoka Uganda, Cindy Sanyu, hatimaye amejibu tetesi zinazomzunguka kuhusu ndoa yake baada ya kuonekana mara kwa mara bila pete ya ndoa. Cindy, ambaye alifunga ndoa na muigizaji na mwongozaji wa filamu Prynce Joel Okuyo mwezi Desemba 2021, amesisitiza kuwa ndoa yake inaendelea vizuri na haina matatizo kama inavyodaiwa. Kwa mujibu wa Cindy, kutoonekana na pete ya ndoa imetokana na tukio ambapo shabiki mmoja aliichukua pete yake wakati wa mawasiliano ya karibu na mashabiki. Ameeleza kuwa kutovaa pete hiyo kumekuwa chanzo cha dhana potofu kuhusu ndoa yake, lakini ukweli ni kwamba uhusiano wake na mumewe unaendelea vizuri na kustawi. Aidha, amesema aliamua kutoanika hadharani tukio hilo ili kulinda ukaribu wake na mashabiki, akihofia kuwa kulizungumzia kungesababisha mpasuko au umbali na wafuasi wake. Kwa ufafanuzi huu, Cindy amewatoa wasiwasi wafuasi wake akisisitiza kwamba ndoa yake na Prynce Joel Okuyo inaendelea kwa mafanikio licha ya tetesi zilizokuwa zikienea.

Read More
 S2Kizzy Atoa Msaada kwa Prodyuza Bakteria Aliyepooza Baada ya Kushambuliwa

S2Kizzy Atoa Msaada kwa Prodyuza Bakteria Aliyepooza Baada ya Kushambuliwa

Mtayarishaji wa muziki kutoka Tanzania, S2Kizzy maarufu Zombie, ameonyesha moyo wa utu baada ya kumtembelea na kumpa msaada prodyuza mwenzake aitwaye Bakteria, ambaye kwa miaka miwili sasa amekuwa akikabiliwa na changamoto kubwa ya kiafya. Katika ziara yake, S2Kizzy alimpelekea msaada wa vyakula na mahitaji ya nyumbani, huku akisisitiza kuwa Bakteria alikuwa tegemeo kubwa kwa familia yake kupitia kazi za muziki, lakini sasa hali ngumu imemlazimisha kusimama. Ameongeza kuwa ni muhimu jamii iungane na kusimama pamoja na wale wanaopitia changamoto. Zombie ametoa wito kwa mashabiki na watu wenye nia njema kushirikiana na kusaidia familia hiyo kupitia namba 0714 315 680. Bakteria alipata matatizo ya kupooza na kushindwa kutembea kufuatia shambulio la vibaka karibu na studio yake mjini Tanga, jambo lililosimamisha kabisa ndoto zake za muziki. Kwa sasa, Bakteria anaishi na mama yake mzazi ambaye pia anakabiliwa na matatizo ya kiafya, hali inayoongeza ugumu wa maisha yao.

Read More
 Pendekezo la Timu 64 Katika Kombe la Dunia 2030 Lateka Vichwa vya Habari

Pendekezo la Timu 64 Katika Kombe la Dunia 2030 Lateka Vichwa vya Habari

Suala la kuongeza idadi ya timu shiriki katika fainali za Kombe la Dunia hadi kufikia 64 limeibuka tena, kufuatia kikao kati ya maafisa wakuu wa CONMEBOL shirikisho la soka la Amerika Kusini na uongozi wa FIFA, ambapo pendekezo hilo liliwasilishwa rasmi kwa ajili ya michuano ya mwaka 2030. Kwa sasa, Kombe la Dunia la mwaka 2026 tayari limepangwa kushirikisha timu 48, lakini CONMEBOL inaamini kuwa wakati umefika wa kuongeza tena idadi hiyo hadi timu 64, ili kutoa fursa kwa mataifa mengi zaidi kushiriki katika tamasha hilo kubwa la kandanda duniani. Kwa mujibu wa taarifa zilizotolewa, pendekezo hilo liliwasilishwa kwa mara ya kwanza katika mkutano wa baraza la FIFA mwezi Machi, na kuungwa mkono na Ignacio Alonso, rais wa shirikisho la soka la Uruguay. Alonso alisisitiza kuwa hatua hiyo itaongeza ushindani na kuifanya michuano hiyo kuwa ya kipekee kwa maadhimisho ya miaka 100 tangu kuanzishwa kwa Kombe la Dunia. Fainali za mwaka 2030, ambazo ni za kihistoria kwa kuwa ni karne moja tangu fainali za kwanza kuandaliwa mwaka 1930 nchini Uruguay, zimepangwa kufanyika kwa ushirikiano wa Uhispania, Ureno na Morocco. CONMEBOL inatumai kuwa kwa kuwa wenyeji watakuwa zaidi ya mmoja, ongezeko la timu litaleta uwiano wa kisiasa, kijiografia na kiushindani katika mashindano hayo. Kwa muktadha wa kihistoria, idadi ya timu katika Kombe la Dunia imekuwa ikiongezeka kadri muda unavyosonga. Mwaka 1982, idadi ya timu iliongezwa hadi 24, na kisha 32 mwaka 1998. Ongezeko la sasa kutoka 48 hadi 64 linaonekana kuwa hatua inayofuata kiasili, hasa kwa kuzingatia ongezeko la mataifa wanachama wa FIFA na ubora unaoendelea kuongezeka duniani kote.

Read More
 Instagram Yaingia Kundi la Apps Zenye Watumiaji Bilioni 3

Instagram Yaingia Kundi la Apps Zenye Watumiaji Bilioni 3

Mtandao wa kijamii wa Instagram umetangaza rasmi kuwa sasa umefikisha wastani wa watumiaji bilioni 3 kwa mwezi, hatua kubwa inayoiweka kwenye orodha ya apps tatu pekee duniani kufikia kiwango hicho cha juu cha matumizi. Instagram sasa inaungana na Facebook na WhatsApp, ambazo pia zinamilikiwa na kampuni ya Meta, katika “chama cha Bil 3”, kundi la majukwaa ya kidijitali yanayotumika na zaidi ya watu bilioni 3 kila mwezi. Facebook ilikuwa ya kwanza kufikia idadi hiyo, ikifuatiwa na WhatsApp ambayo ilifikia watumiaji bilioni 3 mwezi Mei 2025. Kwa upande wake, Instagram ilikuwa na bilioni 2 Desemba 2021, na sasa imeongeza watumiaji bilioni moja zaidi ndani ya kipindi cha takribani miaka minne. Kufikia mafanikio haya makubwa, Instagram imeendelea kuvutia watumiaji kupitia huduma mpya kama Reels, maboresho kwenye Stories, na uhusiano wa karibu na biashara ndogondogo kupitia vipengele vya e-commerce. Kwa ujumla, mafanikio haya yanaonesha wazi nguvu ya kampuni mama ya Meta, ambayo sasa inadhibiti majukwaa makubwa matatu yenye ushawishi mkubwa zaidi duniani kwenye sekta ya mitandao ya kijamii na mawasiliano ya kidijitali.

Read More