
Msanii na mwigizaji wa muda mrefu, Judith Nyambura maarufu kama Avril, ametoa kauli nzito kuhusu malalamiko ya wasanii wa Kenya kuhusu malipo duni kutoka kwa Chama cha Hakimiliki ya Muziki Kenya (MCSK). Akizungumza katika mahojiano ya moja kwa moja na Buzzroom Kenya, Avril alibainisha kuwa mzizi wa tatizo hauko kwa MCSK pekee kama inavyodhaniwa, bali uko kwa taasisi na mashirika yanayocheza muziki wa Kenya bila kulipa ada za leseni.
Avril alieleza kuwa malipo ya wanachama wa MCSK yanategemea moja kwa moja kiwango cha fedha kinachokusanywa kutoka kwa wadau kama vituo vya televisheni, redio, vilabu vya burudani na waandaaji wa matamasha.
“Sijitetetei wala kuitetea MCSK, lakini tukifanya hesabu, ni vipi taasisi kama MCSK itoe mgao wakati wale wanaopaswa kulipa hakimiliki hawafanyi hivyo?” alisema Avril.
Akitumia takwimu kueleza hali halisi, Avril alisema kuwa licha ya ongezeko la wasanii waliosajiliwa, mapato yanayosambazwa yameendelea kuwa haba. Alifichua kuwa mwaka wa 2023, MCSK ilikusanya KSh139.2 milioni pekee. Kwa wanachama 16,000, kila mmoja alipokea wastani wa KSh8,700 kwa mwaka. Aliongeza kuwa hata katika hali ambapo MCSK ingekusanya KSh1 bilioni, malipo kwa kila msanii bado yangekuwa karibu KSh100,000, kiwango ambacho hakitoshi kugharamia hata mradi mmoja wa muziki.
Kwa mujibu wa Avril, mzigo mkubwa uko kwenye sera hafifu za ukusanyaji wa ada badala ya mfumo wa usambazaji wa mapato.
“Sera za ukusanyaji ndizo zinazofeli mfumo huu, si usambazaji wa mapato,” alisema.
Aidha, alisisitiza kuwa wasanii hawawezi kuendelea kutegemea malipo ya hakimiliki pekee kama chanzo cha kipato.
“Sekta ya ubunifu inahitaji wawekezaji wakubwa na wadau wapya, kwa sababu wasanii hawawezi kuishi kwa kutegemea royalty peke yake,” alihitimisha.
Kauli ya Avril imezua mjadala mpya kuhusu mustakabali wa haki za wasanii nchini, huku wadau wa sekta ya burudani wakihimizwa kuangalia upya sheria na sera ili kuhakikisha wasanii wanalipwa haki zao ipasavyo na tasnia ya muziki inakuwa endelevu.