Google Yaianza Maboresho ya Emoji za Android

Google Yaianza Maboresho ya Emoji za Android

Google imeanza kufanya maboresho ya muundo wa emoji zinazotumika kwenye simu za Android, hatua inayolenga kuzifanya zifanane kwa kiasi kikubwa na emoji za iPhone zinazotumika kwenye mfumo wa iOS. Mabadiliko hayo yameanza kuonekana katika mfumo mpya wa majaribio wa Android 16, ambapo emoji nyingi zimeboreshwa muonekano wake na kufanana zaidi na zile za Apple. Kwa muda mrefu, emoji za Android zimekuwa na muundo wa kipekee, tofauti na za iOS na Microsoft, kwani Google ilikuwa ikisisitiza kuwa na utambulisho wake binafsi. Kwa ujumla, mfumo wa emoji duniani unaruhusu kampuni kuwa na uhuru wa kubuni muonekano wao, mradi maana ya emoji ibaki ile ile. Hii ndiyo sababu emoji za mifumo mbalimbali zimekuwa na mwonekano tofauti, licha ya kuwasilisha ujumbe unaofanana. Kwa maboresho haya mapya, inatarajiwa kuwa Android na iOS zitakuwa na muundo unaofanana kwa kiwango kikubwa, ingawa tofauti ndogo bado zitabaki, hususan katika rangi za emoji. Asilimia kubwa ya muundo wake itafanana, jambo linalolenga kuboresha mawasiliano ya kidijitali kwa watumiaji. Hatua hii ya Google imezua mijadala mitandaoni, baadhi ya watumiaji wakifurahia mabadiliko hayo kwa urahisi wa mawasiliano, huku wengine wakieleza wasiwasi wa kupotea kwa utofauti wa muundo wa Android. Maboresho haya yanatarajiwa kuonekana rasmi pindi Android 16 itakapotolewa kwa umma.

Read More
 Google Yazindua Kipengele Kipya cha Recovery Contacts kwa Usalama wa Akaunti

Google Yazindua Kipengele Kipya cha Recovery Contacts kwa Usalama wa Akaunti

Google imeanzisha kipengele kipya kiitwacho Recovery Contacts, kinacholenga kusaidia watumiaji wa huduma zake kurejesha akaunti zao kwa urahisi zaidi endapo watakumbwa na changamoto kama kupoteza simu, kuibiwa, au kushindwa kutumia namba yao ya simu kupata PIN ya kuingia kwenye akaunti. Kupitia huduma hii mpya, mtumiaji wa akaunti ya Google atakuwa na uwezo wa kuteua rafiki wa karibu au mwanafamilia anayeaminika kuwa kama mtu wa kusaidia katika urejeshaji wa akaunti (account recovery). Mtu huyu ataunganishwa kama “recovery contact”, na ataweza kusaidia mtumiaji kupokea PIN code ya muda ya kusaidia kuingia tena kwenye akaunti. Ni muhimu kufahamu kuwa recovery contact hatakuwa na uwezo wa kuingia kwenye akaunti ya mtumiaji, wala kuona taarifa zozote za ndani ya akaunti hiyo. Jukumu lake litakuwa ni kupokea PIN kutoka Google pale itakapohitajika kusaidia katika mchakato wa urejeshaji. Hatua hii inakuja kama sehemu ya jitihada za Google kuimarisha usalama wa akaunti za watumiaji na kuwasaidia wanaopoteza njia ya kawaida ya kuingia hasa kutokana na ongezeko la matukio ya wizi wa simu na changamoto za kiufundi zinazoweza kuziba njia ya kuingia kwenye akaunti. Kwa sasa, huduma ya Recovery Contacts inapatikana kwa hatua za majaribio kwa watumiaji wa baadhi ya huduma za Google, na inatarajiwa kuenea kwa watumiaji wote duniani katika kipindi kifupi kijacho.

Read More
 Google Yazindua “Calling Card” Kwa Watumiaji wa Android

Google Yazindua “Calling Card” Kwa Watumiaji wa Android

Google imeanza kutekeleza mabadiliko mapya yanayolenga kuboresha uzoefu wa watumiaji wa Android, hususan katika eneo la kupiga na kupokea simu. Kupitia sasisho jipya, watumiaji sasa wanaweza kubadilisha mwonekano wa call screen kwa kutumia kipengele kipya kinachoitwa “Calling Card.” Kupitia Calling Card, mtumiaji anaweza kuchagua aina ya herufi za jina, rangi mbalimbali, picha ya full screen, na kubadilisha jinsi skrini ya simu inavyoonekana pale mtu anapopiga simu. Hii inamaanisha kuwa sasa kila simu inayoingia inaweza kuwa na mwonekano wa kipekee wa kuvutia na wa kibinafsi zaidi. Mabadiliko haya mapya yanaifanya Android kufanana zaidi na mfumo wa iOS wa Apple, ambao kwa muda mrefu umejulikana kwa muonekano wake wa kuvutia wa skrini ya simu za kuingia. Kupitia hatua hii, Google inaonyesha nia yake ya kuleta ubunifu unaowapa watumiaji uhuru zaidi wa kubinafsisha vifaa vyao. Kwa sasa, kipengele hiki kinapatikana kwa baadhi ya watumiaji na kinatarajiwa kusambaa zaidi kwa njia ya update ya Google Phone app katika wiki zijazo. Watumiaji wa Android wanashauriwa kuhakikisha programu zao ziko katika toleo jipya kabisa ili kupata huduma hii mpya ya kuvutia.

Read More
 Google Yazindua Rasmi Pixel 10, Pixel 10 Pro na Pixel 10 Fold

Google Yazindua Rasmi Pixel 10, Pixel 10 Pro na Pixel 10 Fold

Google imezindua rasmi simu tatu mpya za kizazi cha Pixel: Pixel 10, Pixel 10 Pro, na Pixel 10 Fold. Ingawa kwa muonekano hazijabadilika sana ukilinganisha na matoleo ya awali kama Pixel 9, simu hizi mpya zimeboreshwa kwa kiwango kikubwa katika teknolojia ya ndani. Mabadiliko makuu yamefanyika kwenye kamera, ambazo sasa zinasaidiwa na akili bandia (AI) ili kutoa picha bora zaidi, hasa katika mazingira ya mwanga hafifu. Pia, simu hizo zina uwezo wa kurekebisha picha kiotomatiki, kuondoa vitu visivyohitajika, na kutoa video zenye ubora wa juu zaidi kwa kutumia teknolojia ya AI. Google pia imeongeza chip mpya ya Tensor G4, inayowezesha simu kufanya kazi kwa haraka zaidi, kutumia umeme kwa ufanisi, na kuruhusu matumizi mapana ya AI ikiwemo kutafsiri lugha papo hapo, kuandika kwa sauti, na kuhariri picha kwa kutumia maandishi. Simu hizo zinakuja na Android 15 na zinatarajiwa kuingia sokoni mwezi ujao. Kwa mujibu wa Google, watumiaji wa Pixel 10 watapata masasisho ya programu na usalama kwa hadi miaka 7, jambo linaloonesha dhamira ya kampuni kuimarisha maisha marefu ya kifaa na usalama wa watumiaji.

Read More
 Google Yazindua Vids, Jukwaa Jipya la Kutengeneza Video

Google Yazindua Vids, Jukwaa Jipya la Kutengeneza Video

Google imezindua jukwaa jipya la kutengeneza video linaloitwa Vids, likiwa sehemu ya hatua zake za kuimarisha huduma kwa watumiaji wake katika uundaji wa maudhui ya kidijitali. Vids ni jukwaa linalotegemea teknolojia ya akili bandia (AI), na limetengenezwa mahsusi kuwasaidia watumiaji kuunda video kwa haraka, kwa urahisi, na kwa ubora wa kitaalamu hata bila kuwa na ujuzi wa kuhariri video. Kupitia Vids, watumiaji wanaweza kuanzisha mradi wa video kwa kuchagua templeti zilizotayari, kisha kupakia picha, sauti, au vipande vya video, na kuacha AI ikisaidie kupanga na kuhariri muundo wa mwisho. Jukwaa hili pia linafanana na huduma nyingine za Google kama Google Docs na Slides, ambapo watumiaji wengi wanaweza kushirikiana kwenye video moja kwa wakati mmoja. Licha ya kuwa bado ipo kwenye hatua ya majaribio, Google Vids tayari imewavutia watumiaji wa Google Workspace waliopata nafasi ya kuijaribu. Kampuni hiyo imesema inalenga kuipanua huduma hiyo ili kuwafikia watu wengi zaidi katika siku zijazo. Uzinduzi wa Vids umeonekana kama hatua ya Google kujiimarisha katika soko la zana za uhariri wa video, na ushindani wake unalenga majukwaa kama Canva, TikTok Video Editor, na CapCut. Watumiaji wengi mitandaoni wameelezea matumaini kuwa Vids itakuwa suluhisho bora kwa wale wanaotaka kuunda maudhui ya video kwa haraka bila kutumia programu ngumu.

Read More
 Akili Bandia ya Gemini Yaweza Kuona Data Zako Zote za Android

Akili Bandia ya Gemini Yaweza Kuona Data Zako Zote za Android

Kampuni kubwa ya teknolojia, Google, imetangaza mabadiliko makubwa katika utaratibu wa akili bandia yake mpya, Gemini, kwa watumiaji wa simu za Android. Sasa, Gemini itakuwa na uwezo wa kuona na kutumia data kutoka kwa programu nyingine zinazotumika kwenye simu hizo. Mabadiliko haya yanamaanisha kuwa akili bandia ya Gemini itapata ufikiaji mpana zaidi wa taarifa kutoka kwa apps mbalimbali, jambo linalolenga kuboresha uzoefu wa mtumiaji kwa kutoa ushauri, huduma, na muunganisho unaozingatia matumizi halisi ya simu. Google imesema kuwa mabadiliko haya ni sehemu ya jitihada za kuleta maendeleo ya teknolojia ya akili bandia na kuhakikisha Gemini inafanya kazi kwa ufanisi zaidi, huku ikizingatia kanuni za usalama na faragha za watumiaji. Hata hivyo, hatua hii imeibua mjadala kuhusu faragha na usalama wa data kwa watumiaji wa Android, huku wataalamu wa usalama wa mtandao wakitoa onyo juu ya hatari zinazoweza kujitokeza endapo data hizi zitatumika vibaya au zikavamiwa na wahalifu wa mtandao. Google imeahidi kuweka hatua madhubuti za kulinda data za watumiaji na kuhakikisha kwamba ufikiaji wa Gemini unafanyika kwa njia salama, huku ikiwahimiza watumiaji kusasisha programu zao na kufuatilia mabadiliko yoyote. Watumiaji wa Android wanashauriwa kusoma kwa makini masharti na sera za faragha zinazohusiana na matumizi ya akili bandia ya Gemini kabla ya kukubali mabadiliko haya.

Read More
 Android 16 Yaboresha Notifications kwa Kipengele cha Live Updates

Android 16 Yaboresha Notifications kwa Kipengele cha Live Updates

Kampuni ya Google imeongeza kipengele kipya katika toleo jipya la Android 16 kinachoitwa Live Updates, ambacho sasa kinapatikana kwenye sehemu ya Notifications na Lock Screen za simu. Mfumo huu mpya wa Live Updates umeundwa kusaidia watumiaji kufuatilia taarifa zinazoendelea kubadilika kwa wakati halisi, kama vile matokeo ya mechi za moja kwa moja, hali ya trafiki, ratiba za usafiri wa umma, au huduma za usafirishaji kama vile magari ya ride-hailing. Taarifa hizi sasa zinaweza kuonekana moja kwa moja kwenye skrini ya simu hata bila kuifungua. Kwa mfano, mtumiaji anaweza kuona mabadiliko ya moja kwa moja ya alama za mechi au mahali gari lake lilipo bila kulazimika kufungua programu husika. Hii inaleta urahisi mkubwa hasa kwa wale wanaotegemea taarifa za papo kwa hapo katika shughuli zao za kila siku. Google imesema kuwa Live Updates zitafanya kazi kwa kushirikiana na apps mbalimbali zitakazosasishwa kuunga mkono teknolojia hiyo, huku usalama na faragha za watumiaji zikizingatiwa. Kipengele hiki kinatarajiwa kuwavutia sana watumiaji wa Android waliokuwa wakitamani urahisi zaidi katika upatikanaji wa taarifa muhimu kwa wakati unaofaa. Toleo kamili la Android 16 linatarajiwa kusambazwa kwa simu mbalimbali kuanzia mwisho wa mwaka huu.

Read More
 Google Yalipa Fidia ya Kihistoria kwa Matumizi Mabaya ya Data

Google Yalipa Fidia ya Kihistoria kwa Matumizi Mabaya ya Data

Kampuni ya teknolojia ya Google imekubali kulipa fidia ya jumla ya dola milioni 314.6 (sawa na takriban shilingi bilioni 40 za Kenya) kwa watumiaji wa Android katika jimbo la California, Marekani, kufuatia madai ya matumizi mabaya ya data za binafsi. Makubaliano hayo ni sehemu ya suluhu ya kesi ya pamoja iliyowasilishwa mahakamani dhidi ya kampuni hiyo, ambapo ilidaiwa kuwa Google ilikusanya na kutumia taarifa za mahali walipo watumiaji bila ridhaa yao halali. Kwa mujibu wa hati za mahakama zilizotolewa wiki hii, Google ilituhumiwa kwa kushindwa kutoa taarifa za kutosha kwa watumiaji kuhusu jinsi taarifa zao za mahali zinavyokusanywa na kutumiwa kupitia huduma zake mbalimbali, ikiwemo Google Maps na Google Search, hata baada ya watumiaji kuzima huduma za ufuatiliaji wa eneo (location tracking). Mwendesha mashtaka mkuu wa jimbo la California, Rob Bonta, alisema kwamba makubaliano hayo ni ushindi mkubwa kwa haki za faragha za watumiaji. Kwa mujibu wa mkataba wa fidia hiyo, zaidi ya wakazi milioni nne wa California wanaostahili walengwa wa fidia hiyo na wataarifiwa jinsi ya kudai malipo yao. Hata hivyo, kiwango halisi ambacho kila mtumiaji atapokea kitapangwa kulingana na idadi ya waliotimiza masharti ya madai. Hii si mara ya kwanza kwa Google kulazimika kulipa fidia kutokana na masuala ya faragha. Mwaka 2022, kampuni hiyo ililipa dola milioni 391 kwa majimbo 40 ya Marekani kutokana na tuhuma kama hizo. Google bado haijatoa taarifa rasmi kuhusu makubaliano haya mapya, lakini imekuwa ikijitetea kwamba imeboresha sera zake za faragha na kuwapa watumiaji wake udhibiti zaidi wa taarifa zao binafsi.

Read More
 Google Yathibitisha Kutumia Video za YouTube Kuimarisha AI

Google Yathibitisha Kutumia Video za YouTube Kuimarisha AI

Google imethibitisha rasmi kuwa inatumia video kutoka YouTube kama chanzo muhimu cha data katika kufundisha mifumo yake ya akili bandia, ikiwamo akili bandia zake za kisasa Gemini na Veo 3. Kwa mujibu wa Google, video hizi hutoa muktadha halisi wa lugha na tabia za binadamu, jambo linalosaidia mifumo ya AI kuelewa lugha kwa undani zaidi na kutoa majibu yenye mantiki na usahihi. Hii ni sehemu ya mbinu za kisasa zinazolenga kuboresha uwezo wa AI katika kutafsiri, kuandika, na kufanya maamuzi kwa njia bora zaidi. Mifumo ya Gemini na Veo 3 ni miradi mikubwa inayolenga kuleta mapinduzi katika sekta ya akili bandia, huku ikizingatia usalama wa data na kufuata sheria za faragha na haki miliki. Google imeahidi kuendelea kuhakikisha matumizi hayo ya data yanafanyika kwa uadilifu, huku ikizingatia miongozo madhubuti kuhakikisha haki na usalama wa watumiaji. Hii ni hatua kubwa inayowekwa mbele katika maendeleo ya teknolojia za akili bandia, ikionyesha jinsi makampuni makubwa yanavyotumia teknolojia za kisasa kuboresha maisha ya kila mtu.

Read More
 YouTube Kuanzisha Teknolojia ya Veo 3 Kuboresha Shorts

YouTube Kuanzisha Teknolojia ya Veo 3 Kuboresha Shorts

Kampuni ya YouTube imetangaza kuwa itaanza kutumia teknolojia ya akili bandia ya kisasa ya Veo 3, iliyotengenezwa na Google, ili kuboresha uzoefu wa watumiaji ndani ya kipengele chake cha video fupi, YouTube Shorts. Teknolojia ya Veo 3 ni moja ya mifumo ya hali ya juu ya video AI ambayo inaweza kutengeneza, kuhariri na kusanifu video kwa kutumia amri rahisi za maandishi (text prompts), na inatambulika kwa uwezo wake wa kutambua rangi, sauti, muktadha, na mtiririko wa hadithi kwa usahihi wa hali ya juu. Kwa mujibu wa taarifa rasmi kutoka Google, matumizi ya Veo 3 ndani ya YouTube Shorts yanalenga kusaidia watumiaji hasa wabunifu wa maudhui kuunda video zenye ubora wa juu kwa muda mfupi, bila hitaji la vifaa vya gharama kubwa au ujuzi wa kitaalamu wa uhariri. Kupitia ushirikiano huo wa kiteknolojia, watumiaji wa YouTube Shorts wataweza kutumia AI kutengeneza transitions za kitaalamu, kuongeza athari za kuona (visual effects) kwa urahisi, kubadilisha maandishi kuwa video ya kipekee na kuboresha sauti, taa na rangi kiotomatiki. Hatua hii ni sehemu ya juhudi za YouTube kuendelea kushindana na majukwaa kama TikTok na Instagram Reels, na pia kumrahisishia kila mtumiaji kuunda maudhui ya kuvutia kwa kutumia teknolojia ya kisasa.

Read More
 Android 16 Yaleta Mwonekano Mpya wa Sliders katika Simu za Android

Android 16 Yaleta Mwonekano Mpya wa Sliders katika Simu za Android

Kampuni ya Google imezindua mfumo wake mpya wa uendeshaji wa simu, Android 16, ambao umeleta maboresho kadhaa yanayolenga kuboresha uzoefu wa mtumiaji. Miongoni mwa mabadiliko yaliyoonekana na kuvutia watumiaji wengi ni mwonekano mpya wa sliders, vifaa vinavyotumika kuongeza au kupunguza sauti, mwanga wa skrini, na chaguzi nyingine mbalimbali zinazotumia mfumo wa kushusha au kupandisha viwango. Katika Android 16, sliders zimepata muundo wa kisasa zaidi, wenye ufanisi na wa kuvutia. Tofauti na matoleo ya awali, sliders sasa zina uhuishaji (animation) laini zaidi, rangi zinazojibadilisha kulingana na mandhari ya kifaa, na mpangilio unaowezesha matumizi rahisi hata kwa mikono miwili au moja. Sliders hizi pia zina uwezo wa kuonyesha viwango kwa usahihi zaidi, jambo ambalo limepokelewa vyema na watumiaji wa simu hasa wanaotegemea marekebisho ya haraka ya sauti au mwanga. Maboresho haya yanatajwa kuwa sehemu ya juhudi za Google kuleta muundo wa kipekee unaojumuisha urembo, ufanisi na matumizi rafiki kwa mtumiaji (user-friendly interface). Pia, Android 16 inakuja na chaguzi zaidi kwa watengenezaji wa programu (developers) wanaotaka kujumuisha sliders kwenye programu zao huku wakifaidika na muonekano huu mpya wa mfumo. Kwa sasa, Android 16 bado iko kwenye hatua za majaribio (beta), lakini tayari imepokelewa kwa shauku kubwa na watumiaji wachache walio na nafasi ya kuijaribu. Toleo la mwisho linatarajiwa kutolewa rasmi kwa watumiaji wa kawaida mwishoni mwa mwaka huu.

Read More
 Google Yaleta “AI Mode” Katika Search Engine Yake

Google Yaleta “AI Mode” Katika Search Engine Yake

Google imezindua mfumo mpya wa “AI Mode” katika injini yake ya utafutaji, unaowezesha watumiaji kuchat moja kwa moja na Google Search kama wanavyofanya na ChatGPT. Hii inalenga kuboresha uzoefu wa utafutaji kwa kutumia teknolojia ya akili bandia. Kampuni hiyo pia imeongeza mfumo wa kisasa wa AI uitwao Gemini 2.5, ambao una uwezo mkubwa wa kuelewa na kuchakata lugha, hivyo kusaidia kutoa majibu sahihi na ya haraka zaidi kwa watumiaji. Mabadiliko haya ni sehemu ya juhudi za Google kuimarisha huduma zake za utafutaji kwa kutumia AI, huku ikilenga kushindana na majukwaa mengine ya teknolojia kama OpenAI na Microsoft. Mfumo huu mpya unatarajiwa kuanza kupatikana kwa awamu duniani kote. Watumiaji wataweza kutumia AI Mode kusaidia katika shughuli mbalimbali kama kutafuta bidhaa, kupanga ratiba, au kutafuta taarifa kwa haraka zaidi, na hivyo kubadilisha jinsi watu wanavyotumia mtandao katika maisha ya kila siku.

Read More