Polisi Kigoma Wakanusha Taarifa za Msanii Shilole Kupata Ajali
Jeshi la Polisi Mkoa wa Kigoma limekanusha rasmi taarifa zinazosambaa kwenye mitandao ya kijamii, hasa TikTok, zikidai kuwa msanii wa muziki Shilole alipata ajali ya gari na kujeruhiwa akiwa safarini kutoka Mkoa wa Kigoma kuelekea Mkoa wa Dodoma. Katika taarifa kwa umma, Polisi wamesema kuwa hakuna taarifa yoyote ya ajali hiyo iliyowasilishwa katika kituo chochote cha Polisi mkoani Kigoma. Polisi wameeleza kuwa taarifa hizo ni za upotoshaji na hazina uthibitisho wa mamlaka husika. Aidha, Jeshi la Polisi Mkoa wa Kigoma limemshauri msanii Shilole kufika katika kituo chochote cha Polisi na kutoa taarifa endapo ajali hiyo ilitokea, ili uchunguzi wa kina uweze kufanyika na hatua stahiki kuchukuliwa. Awali, taarifa hizo za mitandaoni zilidai kuwa gari aina ya Toyota Alphard aliyokuwa akisafiria msanii huyo, ambalo namba zake za usajili hazikufahamika, liligonga ng’ombe katika eneo la Maragalasi wilayani Uvinza na kusababisha ajali hiyo.
Read More