Dulla Makabila Akataa Kuwaomba Watanzania Msamaha kwa Kujihusisha na Siasa

Dulla Makabila Akataa Kuwaomba Watanzania Msamaha kwa Kujihusisha na Siasa

Msanii wa muziki kutoka Tanzania, Dulla Makabila, amezua mjadala mpana mitandaoni baada ya kukataa kuomba msamaha kwa mashabiki kufuatia wasanii kadhaa kulaumiwa kwa kujihusisha na siasa za uchaguzi zilizoibua utata na machafuko nchini humo. Kupitia ujumbe mrefu na wenye hisia kali, Dulla Makabila amesema kuwa binafsi hataki kuombewa msamaha kwa madai ya kuwakwaza watu kutokana na maisha au mafanikio yake. Dulla amesema kuwa kama mafanikio yake yanawakera baadhi ya watu basi hilo ndilo lengo lake, kwani hana mpango wa kuacha kuwakera leo wala kesho. Ameongeza kuwa Mungu ndiye anayejua aliyopitia, na kama amemjaalia riziki, basi ni halali kwa watu waliomdharau kuhisi maumivu hayo. Dulla amefunguka kuhusu safari yake ngumu ya maisha, akisema aliwahi kufukuzwa nyumba na kutupiwa mali zake nje alipokuwa anatafuta maisha, huku baadhi ya watu wakimcheka. Amesema leo haoni kosa kwa wale waliomcheka kushuhudia mafanikio yake, ikiwemo kununua magari kadhaa, akieleza kuwa hayo ni matunda ya subira na maumivu aliyopitia. Msanii huyo pia amedai kuwa kuna watu ndani ya tasnia wanaoishi naye kwa karibu lakini hawampendi, wakijificha nyuma ya kivuli cha urafiki huku wakipambana kwa siri kumuangusha kimuziki kwa kutumia wasanii wengine. Amesema anawajua lakini hachukulii kwa uzito, bali anaendelea na maisha yake kama kawaida. Akihitimisha ujumbe wake, Dulla Makabila amesema shabiki wa kweli hawezi kuchukizwa na mafanikio ya msanii wake, bali hufurahi mara mbili zaidi anapoona msanii wake akifanikiwa. Kauli hiyo ya Dulla Makabila, imekuja baada ya mdau wa burudani, Majizzo, kuwaomba Watanzania msamaha kwa niaba ya wasanii waliokumbwa na wimbi la kukataliwa na mashabiki kutokana na kuhusika kwao katika kampeni za uchaguzi. Ombi hilo lilionekana kulenga kurejesha uhusiano kati ya wasanii na mashabiki waliovunjika moyo.

Read More
 Dulla Makabila Atoa  Milioni 120 Taslimu  Kusaidia Wasanii wa Singeli

Dulla Makabila Atoa  Milioni 120 Taslimu  Kusaidia Wasanii wa Singeli

Staa wa muziki wa Singeli, Dulla Makabila, ameibua gumzo mtandaoni baada ya kuonekana akiwa na kifurushi cha pesa kinachokadiriwa kufikia Tsh milioni 120, akidai kuwa kiasi hicho kimetengwa mahsusi kwa ajili ya kusaidia wasanii wenzake wa Singeli ili waendelee kusimama imara kwenye game. Kupitia ukurasa wake wa Instagram, Dulla Makabila amechapisha video akionesha fedha hizo huku akiwataka mashabiki kuwataja wasanii wa Singeli wanaohitaji mtaji au uwekezaji ili kuendeleza kazi zao. Amesema lengo lake ni kuinua vipaji na kuhakikisha muziki wa Singeli unaendelea kukua bila wasanii wengi kukata tamaa kutokana na changamoto za kifedha. Dulla pia ametumia nafasi hiyo kuwashukuru wasanii Mbosso na Bien kwa kazi yao ya Power Remix, akisema wimbo huo umekuwa miongoni mwa nyimbo zilizompa motisha na kumchangamsha katika kipindi anachohesabu fedha na kupanga mipango yake ya uwekezaji. Hatua yake imepongezwa na mashabiki na wadau wa muziki, hasa ikizingatiwa kwamba Singeli imekuwa ikikua kwa kasi lakini wasanii wengi bado hukumbana na changamoto za rasilimali. Mashabiki wanatarajia kuona utekelezaji wa ahadi hiyo na namna itakavyobadili maisha ya wasanii wanaochipukia katika miondoko hiyo.

Read More
 Dulla Makabila Aonya Vijana Wanaodharau Wanawake Wavumilivu

Dulla Makabila Aonya Vijana Wanaodharau Wanawake Wavumilivu

Msanii wa Singeli, Dulla Makabila, ametoa ushauri mzito kwa vijana wenzake ambao bado hawajafanikwa kimaisha lakini wako kwenye mahusiano. Kupitia ujumbe wake Instagram, Dulla Makabila amesema kuwa iwapo kijana hana fedha kwa sasa na mwanamke wake anaonyesha uvumilivu na kuendelea kusimama naye, basi asiruhusu kumpoteza mwanamke huyo kwa sababu ya mapungufu madogo aliyo nayo. Msanii huyo, amefafanua kuwa katika safari ya maisha, ni vigumu sana kwa mtu aliyefanikiwa kifedha kugundua mwanamke anayempenda kwa dhati na yupi anayempenda kwa ajili ya pesa zake. Kwa mtazamo wa msanii huyo, mwanamke anayechagua kubaki na mwanaume katika kipindi kigumu cha maisha ni wa thamani kubwa, kwani anathibitisha mapenzi ya kweli na sio ya kimaslahi.

Read More
 Bahati akoshwa na wimbo wa Dullah Makabila, “Pita Huku”

Bahati akoshwa na wimbo wa Dullah Makabila, “Pita Huku”

Mwimbaji nyota wa muziki toka Kenya, Bahati ameonyesha kukoshwa na ubunifu alioutumia staa wa Singeli nchini, msanii Dulla Makabila kwenye video ya wimbo wake mpya Pita Huku ulioibua mijadala juu ya mengi kufuatia yaliyo zungumziwa kwenye wimbo huo. Akiacha koment kwenye video hiyo katika mtandao wa YouTube, ujumbe wa Bahati unasomeka, “Huu ni Ubunifu Kaka Yangu. Hongera kwa Muziki mzuri”. Mbali na Bahati pia na wengine wengi wameacha komenti zao wakiusifia ubunifu uliofanywa kwenye kazi hiyo. Wimbo wa “Pita Huku” ambao umetoka Jumatatu ya wiki hii umefanikiwa kupata mapokezi makubwa kutoka kwa wadau mbalimbali wa muziki pamoja na mashabiki kwa ujumla.

Read More