Dulla Makabila Akataa Kuwaomba Watanzania Msamaha kwa Kujihusisha na Siasa
Msanii wa muziki kutoka Tanzania, Dulla Makabila, amezua mjadala mpana mitandaoni baada ya kukataa kuomba msamaha kwa mashabiki kufuatia wasanii kadhaa kulaumiwa kwa kujihusisha na siasa za uchaguzi zilizoibua utata na machafuko nchini humo. Kupitia ujumbe mrefu na wenye hisia kali, Dulla Makabila amesema kuwa binafsi hataki kuombewa msamaha kwa madai ya kuwakwaza watu kutokana na maisha au mafanikio yake. Dulla amesema kuwa kama mafanikio yake yanawakera baadhi ya watu basi hilo ndilo lengo lake, kwani hana mpango wa kuacha kuwakera leo wala kesho. Ameongeza kuwa Mungu ndiye anayejua aliyopitia, na kama amemjaalia riziki, basi ni halali kwa watu waliomdharau kuhisi maumivu hayo. Dulla amefunguka kuhusu safari yake ngumu ya maisha, akisema aliwahi kufukuzwa nyumba na kutupiwa mali zake nje alipokuwa anatafuta maisha, huku baadhi ya watu wakimcheka. Amesema leo haoni kosa kwa wale waliomcheka kushuhudia mafanikio yake, ikiwemo kununua magari kadhaa, akieleza kuwa hayo ni matunda ya subira na maumivu aliyopitia. Msanii huyo pia amedai kuwa kuna watu ndani ya tasnia wanaoishi naye kwa karibu lakini hawampendi, wakijificha nyuma ya kivuli cha urafiki huku wakipambana kwa siri kumuangusha kimuziki kwa kutumia wasanii wengine. Amesema anawajua lakini hachukulii kwa uzito, bali anaendelea na maisha yake kama kawaida. Akihitimisha ujumbe wake, Dulla Makabila amesema shabiki wa kweli hawezi kuchukizwa na mafanikio ya msanii wake, bali hufurahi mara mbili zaidi anapoona msanii wake akifanikiwa. Kauli hiyo ya Dulla Makabila, imekuja baada ya mdau wa burudani, Majizzo, kuwaomba Watanzania msamaha kwa niaba ya wasanii waliokumbwa na wimbi la kukataliwa na mashabiki kutokana na kuhusika kwao katika kampeni za uchaguzi. Ombi hilo lilionekana kulenga kurejesha uhusiano kati ya wasanii na mashabiki waliovunjika moyo.
Read More