Kelechi Africana Awataka DJs Waheshimu Kazi za Wasanii Kenya
Msanii wa muziki kutoka Pwani, Kelechi Africana, ameonyesha kutoridhishwa na tabia ya baadhi ya madj wanaodhibiti sauti za nyimbo wakati wasanii wanatoa burudani kwa mashabiki zao jukwaani. Kupitia ujumbe wake mitandaoni, Kelechi amesema madj wengi wamekuwa wakipunguza sauti ya playback mara tu msanii anapopanda jukwaani, hali inayowafanya mashabiki kupoteza hamasa. Ameeleza kuwa mara nyingi muziki huwa na sauti kubwa kabla msanii hajaanza kutumbuiza, lakini inapungua ghafla msanii anapoanza kuimba, kisha kurejea juu pindi msanii anaposhuka jukwaani. Kelechi amesema hali hiyo inawadhalilisha wasanii na kuathiri ubora wa maonesho, akisisitiza kuwa yeye na wasanii wengine hulipwa kufanya kazi yao kwa ubora, hivyo madj wanapaswa kuwa waangalifu na kuhakikisha usawa wa sauti wakati wote wa onyesho. Aidha, amehoji kama tatizo hilo linatokana na vifaa vya madj au makusudi, akiwataka kuwa na ushirikiano zaidi na wasanii ili kuinua kiwango cha maonesho ya muziki nchini Kenya.
Read More