Entertainment

Msanii Shilole Asamehe Walioharibu Biashara yake, Asema Hatarudi Nyuma Kisiasa

Msanii Shilole Asamehe Walioharibu Biashara yake, Asema Hatarudi Nyuma Kisiasa

Msanii na mfanyabiashara wa Tanzania, Shilole, amezungumza kwa mara ya kwanza baada ya mgahawa wake maarufu Shishi Food kuchomwa moto na waandamanaji wakati wa vurugu zilizoshuhudiwa nchini hivi karibuni.

Kupitia ujumbe Instagram, Shilole amewatakia pole wote waliofikwa na misiba, majeraha, au hasara kutokana na machafuko hayo, akisisitiza kuwa kurudishiana maumivu si utu na kwamba tofauti za kisiasa haziwezi kuondoa undugu na ubinadamu.

Amesema yeye pia ni mhanga wa fujo hizo baada ya ofisi yake kuchomwa na mali zake kuteketea, huku baadhi ya watu wakifurahia tukio hilo kwa sababu ya msimamo wake wa kisiasa ndani ya chama cha CCM. Hata hivyo, amesisitiza kuwa hajawahi kumtukana wala kumdhuru mtu, bali amekuwa muumini wa siasa anayoamini kwa amani.

Shilole ameongeza kuwa vurugu hazibagui, kwani hata wale wasio na chama wamepata hasara, jambo linaloonyesha kwamba fujo hazina manufaa kwa taifa. Amehimiza wananchi kuacha lawama na kuchagua busara, maridhiano na amani.

Msanii huyo pia amewasamehe wote waliohusika na uharibifu wa biashara yake, akisema kuwa mali zinaweza kurudi, lakini uhai hauna mbadala. Ameendelea kumshukuru Mungu kwa kumlinda na kumuombea Rais Samia Suluhu Hassan pamoja na Serikali yake ili waendelee kuimarisha umoja wa taifa.

Akihitimisha ujumbe wake, Shilole amewataka Watanzania kuchagua amani, umoja na busara, akisisitiza kuwa licha ya hasara kubwa aliyoipata, ataendelea kusimama imara na kuamini katika imani yake ya kisiasa ndani ya chama cha CCM.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *