Msanii wa Bongo Fleva, Marioo, ameibuka na kukanusha vikali madai yanayosambaa mitandaoni kwamba alinunua watazamaji (views) wa YouTube kwa ajili ya wimbo wake mpya Oluwa.
Kupitia mitandao yake ya kijamii , Marioo amesisitiza kuwa idadi kubwa ya watazamaji walioupokea wimbo huo ni halali kabisa na inatokana na mapenzi ya mashabiki wake walio ndani na nje ya Tanzania.
Msanii huyo ameonesha kushangazwa na hali ya wimbo wake kushindwa kuingia kwenye orodha ya Trending YouTube, licha ya kufikisha idadi kubwa ya watazamaji ndani ya muda mfupi.
Marioo amewataka mashabiki na watu wenye uelewa wa masuala ya TEHAMA (IT) kujitokeza kumsaidia kubaini tatizo linalofanya wimbo wake usiingie trending YouTube, licha ya kufanya vizuri kwa upande wa watazamaji.
Kauli ya Marioo imeibua mjadala mpana mitandaoni, ambapo baadhi ya mashabiki wameendelea kumpa moyo na kumpongeza kwa mafanikio ya Oluwa, huku wengine wakijadili kwa kina mfumo wa YouTube na vigezo vyake vya trending.